Episode 23

5 1 0
                                    


Inaendelea… 

Baada ya Mariko kuondoka Mtanzi alibaki kupiga bongo. Alikasirika sana kwa mpango wake wa kumnasa Mariko kutibuka. 

“Hivi huyu jamaa anadhani yeye ni nani? Yeye ni mgeni katika uwanda huu lakini tayari anajifanya kujua sana. Lazima nimweke pahali pake.” Mtanzi alijinenea kimoyomoyo. Akaghairi nia, akatwaa rununu yake ya mkononi na kubonyeza. Akasikiza na akairudisha.

Akiendelea kungoja, Katu alijitosa ofisini mwake. Kumbe alikuwa bado hajaenda nyumbani. Hamu ya kutaka kujua kama Mariko alihadaika ilimzidi. Akaamua ajijulie kabla ya kuondoka.

“Mambo sawa?” Katu aliuliza kwa matumaini.

“Wapi! Fedhuli huyo ana akili.” Mtanzi alijibu kwa ghadhabu.

“Lakini bado hawezi kukushinda. Wewe ni babe wa siasa za Takia. Wewe ndiye wa kusema.” 

“Hivi ninavyoona huyu Mariko ana nguvu sana. Watu wataanza kumfuata na kumpenda. Lazima tufanye kitu kabla mambo hayajaenda segemnege.”

“Hatua gani utachukua?”

“Mariko lazima afanyiwe kazi.” Alikaulisha Mtanzi huku uso umekunjika kwa madadi.

“Kazi! Wamaanisha nini?” Alisaili katu.

Mtanzi akamtazama Katu bila kunena chochote. Bila shaka katu alielewa ni kazi gani aliyoashiria Mtanzi. Ila mara hii uoga ulimpanda kwa wazo hilo.

“Najua hauhitaji ufafanuzi. Kazi ikesha kuisha ujie ujira wako. Unazo siku tatu.” Kisha huyo, Mtanzi akaondoka.
Itaendelea… 

VUTA N'KUVUTE Onde histórias criam vida. Descubra agora